Zaidi ya Milioni 414.9 Zatolewa Kuwasaidia Vijana

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Bi. Concilia Niyibitanga akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu Mfuko wa Maendeleo ya Vijana jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Maendeleo ya Vijana, Dk. Steven Kissuina kushoto ni Ofisa Habari wa Idara ya Habari MAELEZO, Frank Mvungi. Picha na Frank Shija.

Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Bi. Concilia Niyibitanga akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu Mfuko wa Maendeleo ya Vijana jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Maendeleo ya Vijana, Dk. Steven Kissuina kushoto ni Ofisa Habari wa Idara ya Habari MAELEZO, Frank Mvungi. Picha na Frank Shija.

Na Daud Manongi

MFUKO wa Maendeleo ya Vijana (YDF) umeendelea kuwa miongoni mwa fursa zinazowasaidia vijana katika kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira miongoni mwao. Haya yamebainishwa na Msemaji wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Bi. Concilia Niyibitanga wakati akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam ambapo alisema kupitia mfuko huo vijana wanapata mikopo ya riba nafuu na elimu ya ujasiriamali.

Niyibitanga aliongeza kuwa katika mwaka wa fedha wa 2013/2014 Mfuko wa Maendeleo ya Vijana (YDF) umetoa mikopo yenye thamani ya shilingi 415,919,000/= kwa vikundi vya vijana 67 kutoka katika Halmashauri 25 za Tanzania Bara.

“Natoa wito kwa Vijana wote nchini kutumia fursa hii ili kujiletea kipato miongoni mwenu hata hivyo mkumbuke ili mpate mikopo hiyo ni wajibu wenu kuzingatia mambo ya msingi vikiwemo vigezo vya kuwasaidia mpate mikopo hiyo, napenda kuwashauri kutembelea Maofisa Vijana waliopo katika maeneo yenu ili mpate uelewa zaidi,” alisema Bi. Concilia

Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi wa Maendeleo ya Vijana, Dk. Steven Kissui alitoa hamasa kwa vijana wengi nchi kuchangamkia fursa itokanayo na mfuko huo ata hivyo alisisitiza umuhimu wa kuzingatia vigezo na masharti muhimu ambayo Serikali imejiwekea katika kuendesha mfuko huo.

Dk. Kissui alisema kuwa ili kikundi kiwe na sifa ya kupata mkopo kutoka mfuko huo ni lazima kiwe kimekidhi vigezo walau kwa asilimia 76 ya vigezo vyote ambapo alivitaja vigezo hivyo kuwa ni pamoja na usajili wa kikundi, leseni ya biashara, kikundi kuwa mwanachama wa SACCOS ya Vijana ambayo ndiyo itakayokuwa na dhamana ya kutoa mikopo hiyo katika Halmashauri, vigezo vingine ni uhalisia wa mradi, upatikanaji wa soko, utunzaji wa mazingira, uwezo wa kupunguza umaskini, uelewa wa wanakikundi juu ya mradi wenyewe, uwezekano wa mradi kulipa mkopo ndani ya miaka miwili pamoja na uwiano wa mkopo na mradi wenyewe na mwisho ukamilifu wa nyaraka na viambatanisho.

Aidha Dkt Kissui aliongeza kuwa pamoja na ufanisi wa mfuko huo kumekuwa na changamoto ya upatikanaji wa fedha kwani mahitaji yamekuwa ni mengi ukilinganisha na fedha inayopatikana kwa ajili ya mfuko huo.

Mfuko wa Maendeleo ya Vijana (YDF) ulioanzishwa na Serikali mnamo mwaka 1993/94 ukiwa na lengo la kuwasaidia Vijana kupata mikopo yenye masharti nafuu ambapo Serikali kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo mwaka 2013 ilitoa mwongozo unaolenga kuanzisha SACCOSS za Vijana katika Halmashauri zote nchini na kupitia SACCOSS hizo vijana watapokea mikopo yao baada ya kukamilisha taaribu zote za uombaji mikopo hiyo.