Yanga Yachapwa Angola, Ila Wasonga Hatua ya Makundi

yanga

Klabu ya Yanga imefanikiwa kufuzu kwenye hatua ya makundi ya michuano ya CAF kwa mara ya kwanza tangu walipofanikiwa kufanya hivyo kwa mara ya kwanza na ya mwisho mwaka 1998.

Yanga wamefungwa na Sagrada Esparenca kwa bao 1-0 lakini wamefuzu kwa matokeo ya jumla (Sagrada Esparenca 1-2 Yanga) hivyo kikosi cha Hans van Pluijm kinasonga mbele kwenye michuano hiyo ya Afrika.

Mechi ya Yanga dhidi ya Esparanca haikuwa rahisi kama watu wengi walivyotarajia kwasababu hadi kipindi cha kwanza kinamalizika wachezaji wanne wa Yanga walikuwa tayari wameoneshwa kadi za njano.

Haruna Niyonzima, Thabani Kamusoko, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Deogratius Munishi Dida ni baadhi ya wachezaji waliooneshwa kazi za njano kutokana na matukio tofauti ya kinidhamu.

Dida aliibeba Yanga baada ya kudaka mchomo wa penati zikiwa ni dakika za lala salama na kuendelea kuweka Yanga kwenye nafasi nzuri ya kusonga mbele.

Nahodha wa Yanga Nadir Haroub Cannavaro alizawadiwa kadi nyekundu dakika za mwisho kabisa za mchezo huo.

Chanzo: shaffihdauda.co.tz