Wanne wapandishwa kizimbani kwa dawa za kulevya

Na Mwandishi Wetu

RAIA wanne wa mataifa tofauti, jana wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi

Kisutu, kwa kosa la kula njama na kuingiza dawa za kulevya nchini zenye thamani ya sh

bilioni 2.8.

washtakiwa hao ambao ni Dennis Okechukwa, Paul Obi ambao ni raia wa Nigeria, mwingine ni

raia wa Afrika Kusini, Stani Hycenth pamoja na raia wa nchini Pakistan ambaye alitajwa kwa

jina la Shoaib Ayaz, wote walisomewa mashtka mawili mahakamani hapo.

Wakili wa upande wa mashitaka, Prosper Mangamila akisaidina na Biswalo Mganga, walisoma

mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mustapher Syani, ambapo ilidaiwa katika shtaka la kwanza

washtakiwa hao wanatuhumiwa kwa kosa la kula njama.

Mwangamila alidai katika siku tofauti kati ya Septemba 26, mwaka jana na Machi 4, mwaka huu

katika maeneo tofauti katika nchi za Tanzania, Nigeria, Afrika Kusini na katika maeneo

tofauti nchini Pakistan washtakiwa hao walikula njama ya kutaka kusafirisha dawa za kulevya

kwa nia ya kuleta nchini.

Alidai katika shtaka la pili ambalo watuhumiwa hao wanatuhumiwa kusafirisha dawa za kulevya,

ilidiwa Machi 4 mwaka huu, huko Kunduchi Mtongani washtakiwa kwa pamoja waliingiza nchini

dawa za kulevya aina ya Heroine gramu 81,000 zenye thamani ya sh 2,835,000,000.

Wakili anayewatetea washtakiwa hao Braison Shayo, aliiomba mahakama kutoa kibali cha

washtakiwa hao kurudishiwa simu zao ili wawasiliane na ndugu zao kwakuwa washtakiwa hao si

raia wa Tanzania.

Hoja hiyo ilipingwa na mawakili wa upande wa mashitaka, ambapo alidai wakili huyo ametumia

kifungu gani cha sheria na kwamba hakuna sheria inayoruhusu vitu vilivyokamatwa kwa ajili ya

uchunguzi kurudishwa kwa mshtakiwa.

Mganga alidai kimsingi mahakama hiyo haina mamlaka ya kutoa au kuruhusu mali hizo kurudishwa

kwa mshtakiwa kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na mamlaka ya kusikiliza shauri hilo.

Wakili huyo wa upande wa mashtaka aliendelea kudai kifungu 38 cha sheria ya makosa ya

mwenendo wa jinai (CPA), kinamruhusu Polisi kukusanya vifaa ambavyo wanaona vinafaa katika

uchunguzi na kwamba kurudishwa kwa mawasiliano kwa washtakiwa hao kutaharibu mwenendo wa

ushahidi kwakuwa kesi hiyo bado inafanyiwa uchunguzi zaidi.

Mahakama ilitoa uamuzi wake, ambapo ilisema haina mamlaka ya kutoa uamuzi wowote kwa hayo

maombi wanayotaka na kwamba wanaweza kuyapeleka Mahakama Kuu ambayo ndio yenye mamlaka ya

kusikiliza shauri hilo, kesi hiyo imehairishwa hadi Machi 21, mwaka huu.