Wanawake Watakiwa Kugombea Uchaguzi Serikali za Mitaa

Mke wa Rais na Mwenyekiti wa WAMA, Mama Salma Kikwete.

Mke wa Rais na Mwenyekiti wa WAMA, Mama Salma Kikwete.

Na Anna Nkinda – Maelezo, Nachingwea

WANAWAKE nchini wametakiwa kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji utakaofanyika mwishoni mwa mwaka huu ili waweze kuingia katika ngazi ya maamuzi. Mwito huo umetolewa jana na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia wilaya ya Lindi mjini Mama Salma Kikwete wakati akiongea na wanachama wa chama hicho wa wilaya ya Nachingwea waliofika kumpokea mara baada ya kuwasili wilayani humo.

Mama Kikwete ambaye ni Mke wa Rais Dk. Jakaya Kikwete alisema ili jambo linalowahusu wanawake liweze kufanyiwa kazi ni lazima wawepo wanawake wenzao wa kuwapigania na hayo yote yatawezekana kama  watajitokeza kuwania nafasi za uongozi.

“Ni vizuri wanawake tukakaa kwa pamoja na kuangalia maslahi yetu kama wanawake, katika hili hatuwezi kushinda kama siku ya uchaguzi tutakaa majumbani tu na kutegemea watu wengine watuchagulie viongozi ni lazima siku hiyo tuende kupiga kura,” alisema Mama Kikwete.

Alisema CCM imeweza kutekeleza Ilani yake ya mwaka 2005/15 kwa waliyoyapanga na wasiyo yapanga hivyo basi wanachama wa chama hicho wanakila sababu ya kutembea kifua mbele na kutoa mfano kwa mambo yasiyokuwa katika Ilani hiyo ni ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) ambacho hadi sasa kimeshatoa wahitimu wa fani mbalimbali. Kuhusu mapendekezo ya Katiba mpya MNEC huyo alisema haikuwa katika Ilani ya Chama hicho lakini kwa kuwa Mwenyekiti wake Rais Dk. Kikwete ni msikivu aliweza kusikia maoni ya wananchi na kuyafanyia kazi na hapo ndipo mchakato wa kuipata katiba mpya na iliyo bora ukaanza.

Mama Kikwete alisisitiza, “Siku si nyingi rasimu ya katiba iliyopendekezwa itapelekwa kwa wananchi kwa ajili ya kuipigia kura, wakati huo ukifika angalieni maslahi ya Taifa na siyo maslahi yenu binafsi na mpige kura ya ndiyo ili tupate katiba bora”.

Mama Kikwete alikuwa wilayani humo kwa ajili ya kuhudhuria kikao cha kamati ya siasa mkoa, wilaya na makatibu wa CCM kata wilaya ya Nachingwea ambacho kilichojadili mambo mbalimbali yanayohusu chama hicho.