Rwanda Mwenyeji wa Mkutano wa Sayansi EAC

Na Mwandishi Wetu, EANA

WATU wapatao 200 wakiwemo watafiti, wanasayansi na wapanga sera wanatarajiwa kuhudhuria mkutano wa nne wa Afya na Sayansi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) mjini Kigali, Rwanda Machi 27-29, mwaka huu. Kauli mbiu ya mkutano huo wa siku tatu ni : Kipaumbele cha Kanda na matarajio:’’Ushahidi wa kuchukua hatua katika Changamoto za Mabadiliko ya Upatikana Fedha Duniani, Shirika Huru La Habari la Afrika Mashariki (EANA) limeripoti.

Mtaalamu wa Masuala ya Afya wa Benki ya Dunia, Prof. Charles Mugone na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Ulaya inayoshughulikia Masuala ya Afya (EDCTB) ni miongoni mwa wataalamu watakaotoa hotuba za ufunguzi katika mkutano huo.

Mkutano huo utakuwa na vipengele vinavyogawaanyika katika makundi manne ikiwa ni pamoja na Afya ya Mama na Mtoto, Magonjwa yasiyo ya kuambukiza na msongo wa mawazo,Uimarishaji wa Mfumo wa Afya na Ubora wa Utoaji Huduma za Afya.

“EAC inafahamu umuhimu ya kuunganisha nguvu katika kuimarsiha ushirikiano wa kikanda kwenye huduma za afya hususan katika utafiti wa masuala ya afya,’’ alisema Katibu Mkuu wa EAC, Dk. Ruchard Sezibera.

Mkutano huo utatanguliwa na Mkutano wa Pamoja wa Bodi za Wataalamu wa Afya na Mabaraza utakaofanyika kati ya Machi 25 na 26, 2013 na Mkutano wa Tisa wa EAC waBaraza la Sekta ya Afya. Mikutano ya EAC ya Afya na Sayansi huitishwa na Sekretarieti ya EAC na kufanyika ndani ya nchi wanachama kwa mzunguko.

Mkutano wa kwanza wa aina hiyo ulifanyika mjini Kampala, Uganda mwaka 2007,mkutano uliofuata ulifanyika nchini Tanzania mwaka 2008 na nchini Kenya mwaka 2009.