Rais Magufuli Amnasa Aliyeficha Sukari, Awatunuku Kamisheni 586 JWTZ

Rais Dk. John Pombe Joseph Magufuli alipokuwa akizungumza na wananchi wa Arusha wakati akirejea Ikulu ndogo kutokea Chuo cha Mafunzo ya Maofisa wa Kijeshi cha Monduli Mei 7, 2016. Picha na Ikulu.

Rais Dk. John Pombe Joseph Magufuli alipokuwa akizungumza na wananchi wa Arusha wakati akirejea Ikulu ndogo kutokea Chuo cha Mafunzo ya Maofisa wa Kijeshi cha Monduli Mei 7, 2016. Picha na Ikulu.

Rais Dk. John Pombe Joseph Magufuli alipokuwa akizungumza na wananchi wa Arusha wakati akirejea Ikulu ndogo kutokea Chuo cha Mafunzo ya Maofisa wa Kijeshi cha Monduli Mei 7, 2016. Picha na Ikulu.

Rais Dk. John Pombe Joseph Magufuli alipokuwa akizungumza na wananchi wa Arusha wakati akirejea Ikulu ndogo kutokea Chuo cha Mafunzo ya Maofisa wa Kijeshi cha Monduli Mei 7, 2016. Picha na Ikulu.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Dk. John Pombe Magufuli Mei 7 amesema tayari vyombo vya dola vimekamata tani 5,000 za sukari iliyofichwa na mfanyabiashara mmoja huko Tabata Jijini Dar es salaam na pia vimembaini mfanyabiashara mwingine aliyeficha sukari hiyo Jijini Arusha.

“Kweli nitawakomesha hawa, wasije wakanilaumu, haiwezekani ukaficha sukari wakati viwanda vyetu vinatengeneza sukari, kuna mmoja mwingine yupo Arusha hapa, naye ameficha sukari, alienda akanunua kwenye viwanda vya sukari vya hapa akaificha yote, leo ninamshughulikia.

“Kuna mwingine alinunua sukari pale Kilombero zaidi ya tani 3,000 akaficha, na mwingine ameshikwa pale Tabata alikuwa ameficha tani 5,000, na wanasubiri katika mwezi Mtukufu wa Ramadhani ili ndugu zetu Waislamu wapate shida, haya ni mashetani makubwa, unawafichia watu chakula ambacho wanatakiwa kula, lakini nataka niwahakikishie ndugu zangu, hili ni tatizo la muda Tanzania, sukari itapatikana kwa wingi, na itanunuliwa na serikali, tumeshaagiza sukari lakini hatutawapa vibali hawa wafanyabiashara ambao wanatunyonya, tutanunua wenyewe na tutauza bei ya chini, hilo ndio lengo la serikali,” Amesema Rais Magufuli.

Aidha, Rais Magufuli amerejea kauli yake kuwa serikali yake haitawavumilia viongozi na watumishi wa umma ambao wamekuwa wakijihusisha na vitendo vya rushwa na ufisadi, huku akisema ataendelea kutumbua majipu kwa yeyote atakayebainika kuchezea mali za umma ili kulinda maslai ya wengi, hususani watanzania wanyonge.

“Ninafanya kwa niaba yenu, ninafanya kwa niaba yenu, ningekuwa sifanyi kwa niaba yenu, na mimi ningeingia madarakani ningeanza kushirikiana na hao, na wengine walifikiria nitashirikiana nao, wamekwama mimi nitawatumbua kila siku ili Tanzania iwe ya neema iweze kwenda mbele, haiwezekani nchi kama hii tajiri, Tanzanite ipo, dhahabu ipo, wanyama mpaka nyani wameanza kuuzwa, wakimalizika nyani si tutauzwa na sisi ndugu zangu, ni lazima nisimamie hili” amesisitiza Dkt. Magufuli.

Awali kabla ya kuzungumza na wananchi, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Dk. John Pombe Magufuli Jumamosi Mei 7, 2016 amewatunuku Kamisheni Maofisa wapya 586 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kundi la 58/15 waliomaliza mafunzo yao katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli (TMA) Mkoani Arusha.

Maofisa hao wapya wa Jeshi walianza kozi yao Mei 4, 2015 na wamepewa cheo cha Luteni usu. Kati ya maofisa wapya waliohitimu kozi yao, 80 ni madaktari na 6 ni marubani wa ndege waliopata mafunzo yao katika nchi tatu ambazo ni Tanzania, Uganda na Afrika Kusini.

Kabla ya kutunuku Kamisheni kwa maofisa hao, Rais Dk. John Pombe Magufuli amekagua gwaride la maofisa hao wapya na pia amepokea heshima ya gwaride lililopita mbele yake kwa mwendo wa pole na haraka, na baadaye kusikiliza ujumbe juu ya utendaji kazi wa serikali ya awamu ya tano, nidhamu ya kazi na uzalendo kupitia muziki wa bendi na kwaya.

Katika hatua nyingine Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli kwa mara nyingine amelazimika kuzungumza na wananchi wa Arusha Mjini waliokuwa wamezuia msafara wake uliokuwa ukitoka Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi Monduli kwenda Ikulu ndogo ya Arusha, na kuwahakikishia kuwa serikali yake imeanza kuwashughulikia wafanyabiashara ambao wameficha sukari kwa makusudi na kusababisha upungufu wa bidhaa hiyo.