Rais Kikwete awatunuku maofisa wa JWTZ

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Dk. Jakaya Kikwete akifurahi na baadhi ya maofisa wanafunzi aliowatunuku kamisheni Novemba 26, 2011 katika Chuo cha Kijeshi Monduli, Arusha.

Na Mwandishi Maalumu

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Jakaya Kikwete, Novemba 26, 2011, ametunuku kamisheni kwa maofisa wanafunzi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania.

Katika sherehe iliyofanyika kwenye Chuo cha Kijeshi Monduli, Arusha, Rais Kikwete ametoa kamisheni kwa maofisa wanafunzi 506 waliofanikiwa kumaliza mafunzo mafupi ya 27.

Kati ya maofisa hao wanafunzi, 69 ni maofisa wa kike na 437 ni maofisa wa kiume na maofisa wote ni wanataaluma wakawa ni pamoja na walimu 101, maofisa mawasiliano ya umma 54, wataalamu wa utawala 48 na wahasibu 167.

Maofisa wengine walitunukiwa kamisheni katika sherehe za leo ni wataalam wa kilimo 14, wahandisi tisa, wanasheria 52, wanahistoria na utamaduni 12, waandishi wa habari 43, wataalam wa ugavi watatu na waataalam wa sayansi ya mazingira watatu.

Wakati huo huo, Rais Kikwete akutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Kenya, Mheshimiwa Raila Odinga. Viongozi hao wawili wamekutana kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere, Dar es Salaam wakati Rais Kikwete akirejea Dar es Salaam jioni.

Viongozi hao wamezungumzia masuala mbali mbali yanayohusu uhusiano kati ya Tanzania na Kenya na yale ya kikanda.