Mrwanda, Kassim waitwa stars, wazuiliwa kuja

Mchezaji Abdi Kassim

WACHEZAJI Dan Mrwanda na Abdi Kassim ni miongoni mwa wachezaji saba wanaocheza mpira wa kulipwa nje ya nchi walioitwa na kocha wa Taifa Stars, Jan Poulsen lakini tayari timu zao zimekaa kuwaruhusu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam na Ofisa Habari TFF, Boniface Wambura amesema wachezaji hao waliitwa kwa ajili ya mechi ya Taifa Stars dhidi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati itakayofanyika Juni 5 mwaka huu jijini Bangui.

Wambura amesema Klabu ya Dong Tam Long ya Vietnam wanaoichezea wachezaji hao wawili imekataa kuwaruhusu kujiunga na Stars kwa madai iko kwenye hali ngumu katika ligi yao. “Timu hiyo inashika nafasi ya mwisho kwenye ligi ya nchi hiyo inayoshirikisha timu 14, hivyo kudai kuwa wachezaji hao ni muhimu kwao kuwaokoa kutoka mkiani,” alisema Wambura katika taarifa yake.
 
Hata hivyo ameongeza TFF tayari imepinga hatua hiyo ya kuzuiliwa kwa wachezaji hao kwani ni kinyume na Kanuni ya Hadhi na Uhamisho wa Wachezaji (Regulations of Status and Players Transfer), hivyo tutawasilisha malalamiko yetu kwa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA).
 
Wakati huo huo, Wambura amesema tayari Kozi ya Wakufunzi (Instructors) wa Waamuzi wa Mikoa imeanza Juni Mosi jijini Dar es Salaam ikishirikisha wakufunzi 16 kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara.
 
Wawezeshaji katika kozi hiyo itakayomalizika Juni 4 mwaka huu na inayofanyika
Ofisi za TFF ni Hafidh Ally, Leslie Liunda, Joseph Mapunda, Riziki Majala na
Juma Ali David.