Mbunge CCM apewa bendera ya Chadema

Mbunge CCM Shinyanga Mjini, Steven Masele

MBUNGE wa Jimbo la Shinyanga Mjini, Steven Masele (CCM) amelazimika kupokea bendera ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutoka kwa vijana wa Kata ya Ndala walioamua kujiunga na Chama Cha Mapinduzi kwa kile kinachodaiwa wamekosa dira ya muelekeo wa kufanya maendeleo.

Akipokea bendera hiyo badala ya kadi katika mkutano wake wa hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi Ndala, jana mjini hapa Mbunge huyo alisema inashangaza wanasiasa kuwatumia vijana vibaya kwa kuwarubuni huku wakijinufaisha wao.

“Sisi wanasiasa tumekuwa tukiwatumia vijana vibaya hasa vyama vya upinzani kila jambo watakalo lipinga ni kuwashawishi vijana kuandamana na kusababisha madhara na vilio katika familia zao, na huko ni kuwatumia vibaya badala ya kuwafanyia jambo ambalo litawaletea maendeleo kwakuwa walituchagua wao tutatue kero zao kwa kuzisikiliza kama tulivyokuwa tukiwaahidi katika kambeni zetu,” alisema Masele.

Alisema vijana 88 aliowapokea walikuwa hawana kadi za chama walichotoka bali walikuwa kama washabiki tu wa chama na sasa wamekwisha ona chama hicho kuwa hakina dira na kubaki kunufaisha maisha yao viongozi na bila kutamka chochote kwa vijana kama walivyokuwa wakiahidi hapo awali.

Aidha alisema tabia ya vyama pinzani kuchonaganisha wananchi na serikali sio kitu cha busara kwani kuna baadhi ya watendaji sio waaminifu wanakura rushwa na kuichafua serikali ya chama cha mapinduzi kuwa haifai katika uongozi

“Viongozi ambao sio waadilifu mimi sitafanya nao kazi ni bora kama wanatabia hiyo waachie madaraka wengine ambao wachapakazi ili tuendelee kuwatendea wananchi maendeleo wanayoyahitaji bila ya kuwepo kwa ubabaishaji wa aina yeyote” alisema

Wakati huo huo alisikitishwa na kitendo cha baadhi ya madiwani wa upinzani kutoonesha ushirikiano naye kwa kutohudhuria ziara zake za kutembelea kila kata na kudai hali hiyo haimkomoi yeye bali wananchi waliowachagua na kutaka maendeleo ikiwa ni pamoja na kutatua kero zao.

“Mimi nitafanya kazi kama diwani kwa kuleta maendeleo kumekuwa kila mara hali hii inajitokeza kwa madiwani wa upinzani kutoonyesha ushirikiano naye mfano wa kata ya Ibadakuli nilipotembelea hapo hakuonekana na sasa kata ya Ndala diwani na Mwenyekiti wote hawapo sasa nitamueleza nani awaletee maendeleo ikiwa wao hawana ushirikiano na mimi” aliwaeleza wananchi

Alisema kwa sasa mambo ya siasa yamekwisha na kazi iliyobaki ni kuwatekelezea wananchi ahadi wakati wa kampeni wanachokifanya hivi sasa viongozi wa upinzani ni kuleta malumbano yasiyo na msingi kwa wananchi ni kuungana pamoja na kuleta maendeleo.
CHANZO; Jambo Leo