Mahakama Afrika Kuanza Kikao Jumatatu Arusha

Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu(AfCHPR) Jaji Augustino Ramadhani(kushoto) akiwa kwenye mazungumzo na mmoja wa wageni wake.

Rais wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu(AfCHPR) Jaji Augustino Ramadhani(kushoto) akiwa kwenye mazungumzo na mmoja wa wageni wake.

Na Mtuwa Salira, EANA

MAHAKAMA ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu (AfCHPR) inaanza kikao chake cha kawaida cha 36 cha mwaka, kuanzia Machi 9 hadi Marchi 27, mwaka huu, katika makao yake makuu mjini Arusha, Tanzania.

Majaji wa mahakama hiyo pamoja na mambo mengine watapokea na kujadili taarifa za mikutano miwili ya kawaida iliyopita na maombi mengine yaliyokwishawasilishwa mbele ya mahakama hiyo. Pia watajadili maombi ya ushauri, kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na mahakama hiyo na Shirika Huru la Habari la Afrika Mashariki (EANA) kupata nakala yake.

Katika kikao hicho Majaji wamepangiwa pia kutembelea Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) na kupata taarifa fupi kutoka kwa Taasisi ya Kusimamia Mambo Yatakayoachwa na Mahakama mbili za Kimataifa (MICT) ambazo ni ICTR na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Kivita katika Yogoslavia ya Zamani yenye makao makuu nchini Uholanzi (ICTY).

MICT ina matawi miwili, moja mjini Arusha na lingine mjini The Hague, Uholanzi.
Mahakama hiyo ya Afrika ina jopo la majaji 11 kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU) wakiwa wamechaguliwa kutokana na nafasi zao binafsi. Mahakama hiyo hukutano katika vikao vyake vya kawaida mara nne kwa mwaka.

Hadi mwishoni mwa mwezi uliopita, AfCHPR ilikuwa imepokea mashauri 35 na kati ya hayo 20 yalishughulikiwa na kukamilishwa. Rais wa sasa wa Mahakama hiyo ni Jaji Augustino Ramadhani kutoka Tanzania.