Madiwani Chato wagomea kikao wagawanyika


Jengo la Halmashauri ya Chato
Chato

SAKATA la madiwani katika Halmashauri ya wilaya ya Chato mkoani Kagera

la kugoma kuingia kwenye kikao cha Baraza limeingia sura mpya baada ya

baadhi yao kujitenga na kuunda Baraza jipya la muda pamoja na kumchagua

Mwenyekiti wa Halmashauri.

Katika kikao kilichofanyika juzi mjini Chato madiwani hao 14 kutoka

chama cha mapinduzi CCM kwa kushirikiana na wale wa chama cha Demokrasia

na Maendeleo CHADEMA walimchagua, Elias Malando Diwani wa Kata ya

Katende kuwa mwenyekiti wao wa muda.

Aidha madiwani hao katika kikao cha Baraza kilichopita waligoma kuingia

kwenye Baraza wakimtuhumu mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo Hamida

Kwikwega amewaburuza kwa kushindwa kuwapa makabrasha mapema pia na

kushindwa kutoa ufafanuzi juu ya matumizi mabaya ya ujenzi wa mabwawa

ya maji yaliyojengwa chini ya kiwango.

Kufuatia hali hiyo madiwani hao 14 waligoma kuingia na kuwaacha wenzao

12 chini ya Mwenyekiti wa Halmashauri, Maisha Charles diwani wa Kata ya

Kigongo kuendelea na kikao hicho ambacho walikipinga wakidai ni batili

kwa sababu kiliendeshwa chini ya idadi ya theluthi tatu kama ilivyo

kwenye mwongozo wa vikao vya Halmashauri.

Pamoja na madiwani hao kuendesha kikao hicho chini ya mwenyekiti wao

wenzao waliogoma kuingia nao waliendesha kikao chao nje ya ukumbi baada

ya kumchagua mwenyekiti wao na kupitisha maadhimio ya kumkataa

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri na kukataa maadhimio yao

waliyoyapitisha kwenye kikao hicho.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Chato alipotakiwa kuzungumzia hali

hiyo alikiri madiwani hao kukataa kuingia kwenye kikao na baada ya

kugoma waliobaki waliendelea na chini ya Mwenyekiti Charles.

Hata hivyo Kwikwega alisema madiwani hao huenda wakawa na madai ya

msingi kwa kuwa ni wawakirishi wa wananchi huku akisisitiza zaidi wapewe

mafunzo ya kujua sheria za utawala katika halmashauri hali ambayo

itaondoa migogoro isiyokuwa ya lazima.

Pia katika madai ya madiwani waliogoma ni pamoja na Halmashauri hiyo

kupewa hati ya mashaka kutokana na ubadhilifu wa matumizi ya fedha na

tayari katika barua yao ya maadhimio ya kumkataa mkurugenzi huyo

wameambatanisha malalamimko yote kwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera na nakala

yake kuipeleka ofisi ya TAMISEMI.

Mkuu wa mkoa wa Kagera, Mohamed Babu akizungumza kwa njia ya simu na

gazeti hili alikiri kupokea kwa malalamiko hayo na kuongeza kuwa

amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Chato, Hadija Nyembo afuatilie na kumpa

taarifa kamili kwa maandishi ili aweze kulifanyia kazi tatizo hilo.

Baadhi ya madiwani waliogoma kuingia kwenye kikao na kuunda baraza lao

akiwemo Diwani wa Kata ya Bwela, Elam Lubagola pamoja na diwani wa Kata

ya Ilemela, Ismail Ruge wametishia kuachia madaraka kwa kujivua gamba

iwapo wataendelea kupingwa wakati wakitetea maslahi ya wananchi.