Dk. Shein: SMZ imeanza kufanya Mapinduzi ya Kilimo


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akishiriki katika uzinduzi wa Uvunaji wa Mpunga wa mbegu, aina ya NERICA, huko katika shamba la kilimo la Mbegu hiyo Bambi Mkoa wa Kusini Unguja jana. (Picha na Ramadhan Othman, IKULU)

Na Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali

Mohamed Shein amesema lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar la

kufanya Mapinduzi ya kilimo tayari limeanza kutekelezwa na mbegu ya aina

ya NERICA ndio mkombozi wa kufikia lengo hilo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo kwa nyakati tofauti mara baada ya

kushiriki kikamilifu katika uvunaji wa mbegu ya mpunga wa kilimo cha juu

aina ya (NERICA) huko Bambi na uzinduzi za uvunaji mpunga Kitaifa,

huko katika bonde la Kisimamchanga Kiboje Mkwajuni Wilaya ya Kati Mkoa

wa Kusini Unguja.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa mbegu ya aina ya NERICA ni

mkombozi mkubwa katika kufikia malengo yaliokusudiwa katika Mapinduzi ya

Kilimo kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa chakula.

Alisema kuwa Serikali kwa upande wake tayari imeshaanza kutekeleza

Mapinduzi ya Kilimo kwa kuamini kuwa hatua hiyo ni moja ya kupambana na

mfumko wa bei ya vyakula hasa mchele ambao ndio chakula kikibwa hapa

Zanzibar.

Dk. Shein alisema kuwa ongezeko la idadi ya watu hapa Zanzibar tokea

Mapinduzi Matukufu ya Januari mwaka 1964 ambapo idadi ya watu ilikuwa ni

laki 3 na mnamo mwaka 1974 ilikuwa ni laki 640 elfu na sensa ya mwaka

2002 idadi ikafikia milioni 1.2 hatua ambayo nayo imepelekea maongezeko

ya mahitaji yakiwemo chakula.

Kutokana na hatua hiyo, Dk. Shein alisisitiza haja ya kuongeza

uzalishaji wa chakula kwani kwa mujibu wa takwemi inaoneshakuwa mchele

unaotumiwa kwa chakula hapa Zanzibar ni tani 80 elfu lakini

unazozalishwa na wakulima hapa nyumbani ni tani 16 elfu tu na kiasi

chote kilichobaki hununuliwa nje ya nchi, ‘Hii ni mbegu na yule atakae

piga goti ale basi ataharibu”alisisitiza Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein aliwataka wakulima nao kubadilika na kushirikiana

vizuri na wataalamu wa sekta ya kilimo katika kuhakikisha mbegu hiyo ya

aina ya NERICA inaleta tija kwa wakulima na wananchi kwa jumla na

kusisitiza nia ya serikali ya kubadilisha mfumo mzima wa kilimo kwa

kutumia vifaa na nyenzo za kisasa za kilimo ili kuondokana na kilimo cha

kilichopitwa na wakati.

Alisema kuwa serikali kwa mara ya kwanza italeta mashine za kuvunia

mpunga ili wakulima wapate kuvuna kwa tija kwani ni njia moja wapo ya

kuimarisha sekta ya kilimo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa miongoni mwa mikakakti madhubuti

iliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kupitia Wizara yake ya

Kilimo ni kuhakikisha wakulima wanapatiwa mbegu bora, mbolea,

pembejeo, Mabwana Shamba, huduma ya umeme na maji ya kutosha.

Dk. Shein alisema kuwa tayari washirika wa maendeleo nao wanaendelea

kuiunga mkono Zanzibar katika sekta hiyo wakimo Japan, Korea ya Kusini,

Marekani hasa katika mradi wao wa ‘Feed the future’ na wengineo.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa serikali imedhamiria kukiimarisha kilimo

cha aina zote likiwemo zao la karafu, pilipili na nyenginezo pamoja na

kuimarisha mbegu mpya ya muhogo ambayo ipo na kuwaahidi wakulima kuwa

watapewa.

Akiwa katika bonde wa Kisimamchanga akizungumza na wakulima wa bonde

hilo, alitoa pongezi kwa wakulima hao kwa jitihada zao za kuendeleza

kilimo cha mpunga kwa kuongeza mara nne uzalishaji wa mpunga katika

bonde lao kutoka na mradi wa PADEP.

Dk. Shein pia, alitoa pongezi kwa Wizara ya Kilimo kwa kushirikiana

pamoja na wakulima hao katika kufikia lengo hilo “Ili tule ni lazima

tulime”,alisema Dk. Shein.

Alisema kuwa tayari serikali imeshapitisha Sheria ya Usalama wa Chakula

hivi karibuni kwa kuzingatia umuhimu wa uhifadhi wa chakula ambapo

serikali itajenga mahala ya chakula kwa lengo la kuweza kusaidia pale

patakapotokezea uhaba wa chakula.

Pia, Dk. Shein akiwa katika bonde hilo aliwaahidi wakulima hao

kuwajengea njia yao inayotoka barabara kuu hadi bondeni kwa kiwango cha

kifusi, umeme, kuchimbiwa kisimatela la kubebea mizigo, mashine za

kuvunia na iwapo wataalamu watahsuri kujengwa hala la kuhifadhi mpunga,

pia, serikali itajenga.

Naye, Waziri wa Kilimo na Maliasili Mhe. Mansour Yussuf Himid aliwaeleza

Wakulima kuwa katika Bajeti ya Wizara hiyo ya mwaka 2011-2012 itakuwa na

matumaini makubwa na kuleta faraja kwa wakulima wote wa Zanzibar.

Alisema kuwa miongoni mwa malengo na matarajio ni kuhakikisha bei ya

mboleo, mbegu, huduma za matrekta, dawa za kuulia wadudu bei zake

zitakuwa ndogo sana kwani serikali chini ya uongozi wa Dk. Shein

ameshakisikia vilio vya wakulima juu ya bei za mahitaji hao.

Alisema kuwa dhamira ya Wizara ya Kilimo ndani ya miaka mitano ni kulima

hekta 6000 za umwagiliaji maji ndani ya hekta 8521 ambapo kati ya hizo

ni hekta 700 tu ndizo inzolimwa hivi sasa na kueleza kuwa tayari Korea

ya Kusini katika mradi wake italima hekta 2000 na Marekani hekta 2000.

Aidha, alisema kuwa mashamba darasa yataongezwa na kufikia 1200, ambapo

pia mashaba darasa nne za mikarafuu zikiwemo mbili za Unguja na mbili za

Pemba zitaanzishwa ikiwa ni pamoja na kuazishwa kwa mradi mpya utaoweza

kuwakopesha wakulima fedha sanjari na kuliimarisha bonde la Kibonde

Mzungu ili kuweza kuzalisha mbegu za mpunga.

Pia, Mkuu wa Mkoa aliwatoa hofu na kuwataka wakulima wa Bonde la

Kisimamchanga kuendelea kulitumia bonde hilo ambapo tayari limeshapimwa

na Wizara ya Kilimo kwa lengo la kuanza kilimo cha umwagiliaji maji.

Nao wakulima wa bonde la Kisimachanga walieleza kuwa mara baada ya

kuingia katika mradi wa PADEP ambao umetumia zaid ya Shilingi milioni 32

mafanikio makubwa yamepatikana ikiwa ni pamoja na kuongeza uzalishaji wa

mpunga ambapo hivi sasa wanazalisha polo 4 kwa robo hekta ambazo hapo

zamani ndizo walizokuwa wakizalisha kwa hekta nzima.

Katika hafla hiyo ya kitaifa baadhi ya wakulima na viongozi kutoka mikoa

yote mitano ya Unguja na Pemba walihudhuria pamoja na Mawaziri,

Wawakilishi, Mkuu wa Mkoa wa Kusini ambaye n mwenyeji pamoja na Mkuu wa

Mkoa wa Mjini Mgharibi na Kusini Pemba walihudhuria, viongozi wa

serikali na kisiasa, pamoja na wananchi kutoka maeneo mbali mbali

walihudhuria.

Jumla ya heka tano za mbegu ya mpunga wa aina ya NERICA zimevunwa pia

mbegu hizo zinatarajiwa kupandwa kwa wingi katika mvua za vuli

zinazokuja kwa lengo la la kuja kupandwa wakati wa Masika ambapo zaidi

ya tani 3700 za ziada zinatarajiwa kupatikana katika msimu wa masika

ujao lengo ni kufikia asilimia 50 ya uzalishaji ndani ya miaka mitano.