Balozi Sefue Kuzinduwa Mashindano ya SHIMIWI 2015

Katibu Mkuu Kiongozi,Balozi Ombeni Sefue akizungumza.

Katibu Mkuu Kiongozi,Balozi Ombeni Sefue akizungumza.


Na Mwandishi Wetu, MAELEZO-Dar es salaam

KATIBU Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa michezo ya Wizara, Idara zinazojitegemea, Wakala wa Serikali na Ofisi za wakuu wa Mikoa (SHIMIWI) itakayoanza Jumamosi ijayo(15.8.2015) mjini Morogoro.

Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa leo jijini Dar es salaam na Kaimu Katibu Mkuu SHIMIWI Moshi Makuka, mashindano ya mwaka huu yatafanyika kwa wiki mbili.

Amesema kuwa siku ya ufunguzi kutakuwa na michezo ya mpira wa miguu kati ya Elimu na Hazina kwa wanaume, mpira wa pete utazikutanisha timu ya Afya na Mambo ya Ndani.

Makuka ameongeza kuwa siku hiyo pia kutakuwepo mchezo wa kuvuta kamba kati ya Wakala wa Jiolojia Tanzania na Mambo ya Nje kwa wanaume na kamba kwa wananwake kati ya Ikulu na Bunge.

Amezitaja timu zilizothibitisha kushiriki kuwa ni Ikulu, Utumishi, Waziri Mkuu, Afya, Ardhi, Elimu, Hazina, Kilimo, TAMISEMI, Mifugo, Maji, Afrika Mashariki, Maliasili, Mambo ya Nje, Mambo ya Ndani, Ulinzi, Nishati, Maendeleo ya Jamii, Viwanda, Uchukuzi, Ujenzi na Tume ya Mipango.

Timu nyingine ni Mahakama, Tume ya Utumishi wa Umma, Bunge, Tume ya Kurekebisha Sheria, Tume ya Mahakama, Ukaguzi, tume ya ushirika, Wakala wa Jiolojia Tanzania, Wakala wa Ukaguzi wa Madini, Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula, Mkoa wa Lindi, Katavi, Mwanza, Kagera, Rukwa, Dar es salaam, Mtwara, Iringa, Geita, Kigoma, Manyara, Arusha, Mara, na Tanga.