Babu Loliondo afanya maajabu

Mchungaji Mwasapile

Na Mwandishi Wetu,
Loliondo

MIUJIZA ya Mchungaji Ambilikile Mwasapile wa Kijiji cha Samunge, Loliondo wilayani Ngorongoro juzi Ilijidhihirisha kijijini hapa baada ya mmoja wa wezi aliyechomoa pochi ya mgonjwa raia wa Kenya kusalimisha pochi hiyo kwa Mchungaji huku akidai anapigwa na watu asiowaona na kushindwa kuona.

Aprili 2, 2011 mmoja wa raia kutoka nchini Kenya aliibiwa pochi iliyokuwa na fedha za Kenya sh. 20,000, simu, hati ya kusafiria na vitambulisho mbalimbali hali iliyomlazimu kutoa taarifa ya wizi huo kwa Mchungaji Mwasapile akiomba msaada.

Baada ya kutoa taarifa hiyo Aprili 3, majira ya saa saba mchana mchungaji Mwasapila alitangaza kwa watu waliokusanyika kijijini hapo na kutaka aliyeiba arejeshe vitu hivyo na kwamba asipofanya hivyo fimbo ya Mungu itamuadhibu.

“Ndugu zangu wagonjwa, Kijiji cha samunge kimevamiwa na majambazi na wezi ambao wameanza kuwaibia watu, nawaomba walioiba vitu hivyo wavirejeshe na waondoke kwa amani katika Kijiji hiki haraka kabla Mungu hajaanza kuwaadhibu kwa mkono wake,” alisikika akiwatangazia wananchi.

Katika hali isiyokuwa ya kawaida wakati watu waliokuwa wamefurika wakianza kupata dawa ghafla vijana wawili wakiwa wamefuatana na mama mmoja ambae jina lake halikufahamika mara moja walifika eneo la Mchungaji Ambilikile anakotolea dawa na kuomba msaada wake kuhusu kijana aliyekuwa analalama kuwa anapigwa na ambao hawaoni.

Kufutia hali hiyo, mchungaji Mwasapile alimwambia Kijana huyo aliyejulikana kwa jina moja la Joseph asalimishe vitu vyote alivyoviiba na kisha ampe dawa na baada ya kutoa simu aina Black Berry, fedha Sh. 20,000 za Kenya, hati ya kusafiria sh. 80,000 za Tanzania mchungaji alimmwagia dawa na ghafla alianza kuona na kuacha kupiga kelele.

Imebainika kijana huyo aliyefahamika kwa jina moja la Joseph (28) alikuwa ametokea mkoani Singida na Mama yake ambaye ni mchuuzi wa Chakula eneo hilo.