Soma Washindi wa Tuzo za Ligi Kuu Tanzania Bara

VPL

BEKI wa Yanga, Juma Abdul Jaffar Mnyamani ameshinda tuzo ya Mchezaji Bora wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara msimu wa 2015/2016.

Katika sherehe za utoaji wa tuzo hizo usiku huu ukumbi wa Double Tree Hotel By Hilton, Masaki, Dar es Salaam, Abdul ambaye pia ni mchezaji wa timu ya taifa, Taifa Stars amewashinda beki mwenzake, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ wa Simba na kiungo wa Mtibwa Sugar, Shizza Kichuya.

Na kwa ushindi huo, Abdul mbali na kukabidhiwa taji na mgeni rasmi, Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwigulu Nchemba, pia atazawadiwa fedha Sh Milioni 9.2 wakati klabu yake, Yanga SC itazawadiwa Sh. Milioni 81.3 kwa kuwa bingwa, huku Sh. Milioni 40.6 zikienda kwa washindi wa pili, Azam FC, Sh Milioni 29 zikienda kwa washindi wa tatu, Simba SC na Sh. Milioni 23.2 zikienda kwa Prisons washindi wa nne.

Aishi Salum Manula wa Azam FC ameshinda tuzo ya kipa Bora akiwaangusha Deo Munishi ‘Dida’ wa Yanga na Benno Kakolanya wa Prisons na kuzawadiwa Sh. Milioni 5.7 huku mfungaji bora Amissi Tambwe wa Yanga akizawadiwa pia Sh. Milioni 5.7.

Thabani Michael Kamusoko ameshinda tuzo ya Mchezaji Bora wa Kigeni, akiwaangusha Mzimbabwe mwenzake anayecheza naye Yanga SC, Donald Ngoma na kipa Muivory Coast wa Simba, Vincent Agban hivyo kuzawadiwa Sh. Milioni 5.7 pia.

Mholanzi Hans van der Pluijm ameshinda tuzo ya Kocha Bora na kuzawadiwa Sh. Milioni 8, akiwaangusha Mecky Maxime wa Mtibwa Sugar na Salum Mayanga wa Prisons.

Tshabalala ameshinda tuzo ya Mchezaji Bora Chipukizi akiwaangusha Farid Mussa wa Azam na Shizza Kichuya wa Mtibwa Sugar na kuzawadiwa Sh. Milioni 4.

Ibrahim Hajib wa Simba ameshinda tuzo ya Bao Bora la Msimu na kuzawadiwa Sh. Milioni 3 akimuangusha Tambwe wa Yanga, wakati Mtibwa Sugar imezibwaga JKT Ruvu na Mgambo Shooting katika tuzo ya Timu yenye Nidhamu na kuzawadiwa Sh. Milioni 17.2.

Ngole Mwangole ameshinda tuzo ya Refa Bora na kuzawadiwa Sh. Milioni 5.7 baada ya kuwaangusha Anthony Kayombo na Rajab Mrope.

chanzo:binzubeiry.co.tz