Waziri Nape Awasimamisha Kazi Watendaji wa TBC

Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Nape Moses Nnauye akipokelewa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) Bw. Clement Mshana alipowasili katika ofisi za TBC Mikocheni leo jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, Nape Moses Nnauye akipokelewa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) Bw. Clement Mshana alipowasili katika ofisi za TBC Mikocheni leo jijini Dar es Salaam.

Na Frank Shija, WHUSM

WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amewasimamisha kazi watumishi wawili wa Shirika la Utangazaji la Taifa TBC kutokana na utendaji usioridhisha.
Akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za TBC leo jijini Dar es Salaam, Waziri Nape amewataja watumishi waliosimamishwa kazi kuwa ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari na Matukio Bwana Mbwilo Kitujime na Meneja wa Vipindi Bibi. Edna Rajab ambao wote kwa pamoja wamesimamishwa kazi na uamuzi huo utafikishwa kwa Bodi ya TBC kwa hatua zaidi.
“Tunachukua uamuzi wakuwasimamisha kazi watendaji hawa ili kujenga upya Idara hii muhimu katika ustawi wa TBC na habari kwa ujumla.” Alisema Nape
Aidha Waziri huyo amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa TBC kuwachukulia hatua watumishi wengine walio chini ya Idara hiyo kwa kuwa wako chini ya mamlaka yake na kutoa mrejesho wa hatua alizochukua dhidi ya wale wote wilioonesha utendaji mbovu.
Alisema kuwa Serikali imefikia uamuzi huo kutokana na kuwepo kwa malalamiko ya muda mrefu juu ya utendaji mbovu na wakutoridhisha viongozi na baadhi ya watumishi wa Idara hiyo hiyvo hatua hizo zimechukuliwa ikiwa ni kujenga upya na kuboresha Idara hiyo muhimu katika uendeshaji wa Shirika lolote lile la Habari na kuongeza ufanisi.
Idara ya Habari na Matukio ya TBC inaundwa na Mkurugenzi wa Idara, Meneja wa Vipindi Wahariri na Waandishi wa Habari ambapo tayari Mkurugenzi na Meneja wa Vipindi wamesimamishwa kazi leo tarehe 15 Februari 2016 na watumishi wengine watachukuliwa hatua kufuatia agizo la Mhe. Waziri wa Habari kwa Mkurugenzi Mkuu wa TBC alilolitoa leo wakati akitangaza kuwasimamisha kazi viongozi hao.