TANESCO Yatoa Tahadhari Waharibifu Vyanzo vya Maji

Msemaji wa Wizara ya Nishati na Madini Bi. Badra Masoud akiwaeleza waandishi wa habari (hawapo pichani)mapema leo jijini Dar es Salaam kuhusu mpango wa Serikali wa kuunda kikosi maalum cha kukabiliana na tatizo la wizi wa umeme na kuimarisha ukaguzi ili kubaini wateja wasio waaminifu na kuwachukulia hatua za kisheria. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari (MAELEZO) Bi. Zamaradi Kawawa. (Picha na Fatma Salum- Maelezo)

Msemaji wa Wizara ya Nishati na Madini Bi. Badra Masoud akiwaeleza waandishi wa habari (hawapo pichani)mapema leo jijini Dar es Salaam kuhusu mpango wa Serikali wa kuunda kikosi maalum cha kukabiliana na tatizo la wizi wa umeme na kuimarisha ukaguzi ili kubaini wateja wasio waaminifu na kuwachukulia hatua za kisheria. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari (MAELEZO) Bi. Zamaradi Kawawa. (Picha na Fatma Salum- Maelezo)


Na Jovina Bujulu – Maelezo

MABADILIKO ya Tabia Nchi, uharibifu wa vyanzo vya maji katika mito mbalimbali na uchepushaji wa maji kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji ni chanzo cha kukauka kwa mabwawa ya maji yanayotumika katika kuzalisha umeme.
Hayo yamesemwa jijini Dar es salaam na msemaji wa Wizara ya Nishati na Madini Bi. Badra Masoud alipokuwa akizungumzia ukaguzi wa wezi wa umeme nchini.

“Umeme unaotumika kwa sasa unazalishwa kwa kiasi kikubwa na gesi asilia pamoja na mafuta mazito na diseli ambapo umeme unaotokana na nguvu ya maji unazalishwa kwa kiasi kidogo,” alisema Bi Badra.

Akizungumzia hali ya umeme nchini, Badra alisema kwamba kwa sasa hakuna mgawo wowote unaoendelea kwani uzalishaji ni mzuri, kiasi cha umeme kinachopatikana sasa ni megawati 1500 wakati matumizi kwa siku ni megawati kati ya 800 na 900.

Aidha Bi. Badra alisema kwamba Wizara ya Nishati na Madini inatarajia kuunda kikosi maalumu kitakachojumuisha wataalamu kutoka katika taasisi mbalimbali kukabiliana na wizi wa umeme nchini.

“Wizi wa umeme nchini ni jambo linalolikosesha mapato shirika la Tanesco, hivyo kikosi hicho kitajumuisha wataalamu kutoka TANESCO, Wizara ya Nishati na Madini pamoja na vyombo vya usalama” alifafanua Bi Badra.

Pia Wizara imewataharisha baadhi ya watu wanaohujumu miundombinu ya TANESCO kama kuchoma nguzo za umeme, kuiba mafuta ya transforma pamoja na nyaya za umeme na watakaogundulika watachukuliwa hatua za kisheria.

Hata hivyo Shirika la umeme Tanzania TANESCO limeagizwa kuimarisha kikosi chake cha ukaguzi wa watumiaji wa umeme ili kubaini wateja wasio waaminifu wanaoiba umeme wa majumbani na viwandani na kuwachukulia hatua za kisheria.

Katika kuhimiza matumizi bora ya umeme Wizara ya Nishati na Madini imezitaka taasisi mbalimbali za serikali na zisizo za kiserikali kuzingatia matumizi mazuri ya Nishati hiyo ili kudhibiti upotevu wa umeme.