JK Ateuwa Wenyeviti na Makamishna Tume ya Haki za Binadamu

Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete.

Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete.


RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, amefanya uteuzi wa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Makamishna wanne wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kama ifuatavyo:-

Mwenyekiti:
Bwana Bahame Tom Mukirya -NYANDUGA Ana Shahada ya Sheria, 1977 (Dar es Salaam), Shahada ya Uzamili ya Sheria, 1987, (London) na Diploma ya Uzamili ya Sheria, 1981 (The Hague). Alifanya kazi Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa wa Kimataifa kwa miaka 17. Alikuwa Rais wa Chama cha Mawakili wa Kujitegemea wa Tanganyika, 2001-2009. Alikuwa Kamishna wa Umoja wa Afrika wa Kamisheni ya Haki za Binadamu (2003-2009). Ni Mtaalam Huru wa Somalia wa Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu, (2014).

Makamu Mwenyekiti:
Bwana Iddi Ramadhani MAPURI – Ana Shahada ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, 1984 na Diploma ya Uzamili ya Maendeleo Vijijini, 1987 na Diploma ya Uzamili ya Menejimenti (India). Alikuwa Kamishna wa Kazi, 1989-2010. Ni Mkurugenzi wa Utawala na Maendeleo ya Rasilimali Watu katika Wizara ya Vijana, Wanawake na Uwezeshaji tangu 2011.

Makamishna:
1. Bwana Mohamed Khamis HAMAD – Ana Shahada ya Sheria, 2004 (Zanzibar), na Shahada ya Uzamili ya Sheria 2007 (Oslo). Ni Wakili wa Serikali Mwandamizi katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka. Alikuwa Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Rufani za Kodi. Alikuwa pia Mkuu wa Kitengo cha Utafiti, Tume ya Kurekebisha Sheria.
2. Dkt. Kevin MANDOPI -Ana Shahada ya Sheria, 2003 (Dar es Salaam), Shahada ya Uzamili ya Sheria, 2007 (Dar es Salaam) na Shahada ya Uzamivu, 2013 (St. Augustine University), Mwanza. Ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Msaada wa Sheria, Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto. Ni Wakili wa Kujitegemea tangu 2005. Ni Mhadhiri wa Sheria.
3. Bibi Rehema Msabila NTIMIZI
Ana Shahada ya Sheria, 2001 (Dar es Salaam) na Shahada ya Uzamili ya Sheria, 2003 (Dar es Salaam). Alikuwa Wakili Mkuu wa Serikali 2005-2007; Kaimu Msaidizi Mwandamizi wa Msajili wa Hati, Wizara ya Ardhi, 1994-2005. Ni Meneja wa Ulinzi wa Mali Vijijini, MKURABITA, (tangu 2008).
4. Bibi Salma Ali HASSAN -Ana Shahada ya Sheria, 2001 (Malaysia) na Shahada ya Uzamili ya Menejimenti, 2009 (Malaysia). Alikuwa Wakili wa Serikali, 2002-2009, Afisa wa Haki za Binadamu, Wizara ya Katiba na Utawala Bora. Ni Wakili wa Kujitegemea tangu 2011. Uteuzi huo unaanzia tarehe 06 Januari, 2015, na wataapishwa Ikulu, Dar es Salaam siku ya Alhamisi, tarehe 8 Januari 2015, saa sita adhuhuri.

Imetolewa na;
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
07 Januari, 2015