Sitta Avitaka Vyombo vya Habari Kuacha Uchochezi

Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta akiongea na waandishi wa Habari huku akiwaasa kuacha chuki katika masuala yanayohusu mchakato wa Katiba. (Picha zote na Benedict Liwenga, Maelezo-Dodoma)

Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta akiongea na waandishi wa Habari huku akiwaasa kuacha chuki katika masuala yanayohusu mchakato wa Katiba. (Picha zote na Benedict Liwenga, Maelezo-Dodoma)


Mjumbe wa Kamati Namba Moja ya Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Ummy Mwalimu Ally akiongea na wandishi wa Habari kuhusu kazi na majukumu ya Kamati yake leo 28 Agosti, 2014.

Mjumbe wa Kamati Namba Moja ya Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Ummy Mwalimu Ally akiongea na wandishi wa Habari kuhusu kazi na majukumu ya Kamati yake leo 28 Agosti, 2014.

Na Benedict Liwenga, Maelezo – Dodoma

MWENYEKITI wa Bunge Maalum la Katiba, Samuel Sitta amevitaka vyombo vya habari nchini kuacha uchochezi na chuki wakati vinapohabarisha umma kuhusiana na mchakato wa Katiba Mpya. Kauli hiyo nimetolewa na Sitta wakati alipokutana na baadhi ya waandishi wa habari katika viwanja vya Bunge mjini Dodoma huku akiviasa vyombo vya habari kuachana na kuandika habari zenye kuleta uchochezi na chuki ili kuvuruga mchakato wa Katiba Mpya.

Sitta alisema kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa na dhana tofauti kuhusu kazi ifanywayo na Bunge Maalum la Katiba, hivyo ni vema kuepukana nao na kuhabarisha umma taarifa sahihi ili Katiba Mpya iweze kupatikana.

“Kusema tunafanya kazi ya Tume ni upotoshaji mkubwa, sisi tunafanya kazi tuliyotumwa tena kwa uadilifu mkubwa. Upotoshwaji mwingine unafanywa na baadhi ya watu ambao hawalitakii mema Taifa letu na hawapendi kuona mchakato wa Bunge la Katiba unaendelea vizuri,” alisema Sitta.

Sitta aliongeza kwa kutolea ufafanuzi juu ya baadhi ya makundi yaliyowasilisha mapendekezo yao katika Bunge hilo, kwa kusema kuwa maoni yanayoletwa na makundi mbalimbali kwa lengo la kuboresha Rasimu Mpya ya Katiba yanapokelewa lakini sio maoni tu ya mtu binafsi au mwananchi, bali wanapokea maoni kupitia makundi maalum kama yalivyo kwa wafugaji, Wasanii na Wakulima ambao wameshawahi kuwasilisha maoni na mapendekezo yao katika iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba lakini hayakuonekana na mengine yalisahaulika katika Rasimu hiyo.

“Tuna haki na wajibu wa kuyapokea makundi haya ili kutoa Katiba iliyo rafiki kwa wananchi wote,” alisisitiza Sitta.

Wakati huo huo, baadhi ya Wenyeviti wa Kamati mbalimbali za Bunge hilo, wamesema wamemaliza kazi ya kuchambua Rasimu hiyo vizuri katika Kamati zao. Akizungumzia kuhusu kazi hiyo, Mwenyekiti wa Kamati Namba Tatu ya Bunge hilo, Dk. Francis Michael amesema suala la ardhi lilionekana kuwa nyeti katika Kamati yake.

Dk. Francis aliongeza kuwa suala la kupokea mapendekezo kutoka kwa makundi mbalimbali si kwamba kila kitu kitawekwa kwenye Katiba Mpya bali ni yale mambo ya msingi.

Naye Mwenyekiti wa Kamati Namba Moja ya Bunge hilo, Ummy Mwalimu Ally na Makamu Mwenyekiti wa Kamati Namba Kumi na Moja, Hamad Massauni walisema kuwa katika Kamati zao majadiliano yalikwenda vizuri.