Ligi Kuu Tanzania Bara Kutimua Vumbi Sep 20

Kombe la Ligi Kuu Tanzania Bara

Kombe la Ligi Kuu Tanzania Bara

MICHUANO ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kuwania ubingwa wa Tanzania Bara msimu wa 2014/2015 itaanza kutimua vumbi Septemba 20 mwaka huu. Awali michuano hiyo ilikuwa ianze Agosti 24 mwaka huu, lakini Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania limelazimika kuisogeza mbele kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kupitisha michuano ya klabu bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame).
 
Michuano ya Kombe la Kagame inayoshirikisha mabingwa wa nchi wanachama wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) itafanyika Agosti mwaka huu nchini Rwanda.
 
Timu 14 zitashiriki Ligi Kuu msimu huu. Timu hizo ni mabingwa watetezi Azam, Coastal Union, JKT Ruvu Stars, Kagera Sugar, Mbeya City, Mgambo Shooting, Mtibwa Sugar, Ndanda FC, Polisi Morogoro, Ruvu Shooting, Simba, Stand United, Tanzania Prisons na Yanga. Ratiba ya ligi hiyo itatolewa mwezi mmoja kabla ya michuano hiyo kuanza kutimua vumbi.