Dk Bilal Aanza Ziara ya Kikazi Nchini Japan

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohammed Gharib Bilal, akibadilishana zawadi na Waziri wa Biashara, Uchumi na Viwanda wa Japan, Toshimitsu Motegi, baada ya mazungumzo yaliyofanyika ofisini kwa Waziri huyo akiwa katika ziara yake nchini Japan, Mei 20, 2014.Picha OMR

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohammed Gharib Bilal, akibadilishana zawadi na Waziri wa Biashara, Uchumi na Viwanda wa Japan, Toshimitsu Motegi, baada ya mazungumzo yaliyofanyika ofisini kwa Waziri huyo akiwa katika ziara yake nchini Japan, Mei 20, 2014.Picha OMR

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohammed Gharib Bilal, akiwa katika mazungumzo na Mwenyekiti wa Kampuni ya JETRO, Hiroyuki Ishige, wakati walipokutana na kwa mazungumzo akiwa katika ziara yake nchini Japan, Mei 20, 2014. Picha OMR

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohammed Gharib Bilal, akiwa katika mazungumzo na Mwenyekiti wa Kampuni ya JETRO, Hiroyuki Ishige, wakati walipokutana na kwa mazungumzo akiwa katika ziara yake nchini Japan, Mei 20, 2014. Picha OMR

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameanza leo ziara ya Kikazi nchini Japan, ziara inayolenga kuongeza ushirikiano baina ya Japan na Tanzania ikizingatia maeneo ya uwekezaji na ubadilishaji wa teknolojia baina ya nchi hizi mbili. Makamu wa Rais baada ya kuwasili nchini hapa na kukutana na viongozi wa Ubalozi wa Tanzania nchini Japan ulio chini ya Balozi Salome Sijaona, alianza ziara hiyo kwa kutembelea Ofisi ya Wizara ya Biashara Uchumi na Viwanda na kukutana na Waziri wa Wizara hiyo Mheshimiwa, Toshimitsu Motegi, ambaye alimfahamisha Mheshimiwa Makamu wa Rais kuhusu maeneo ambayo Japan imekuwa ikishirikiana na Tanzania, sambamba na yale ambayo ingetarajia kushirikiana zaidi katika siku zijazo. 

Akiwa wizarani hapo Mheshimiwa Makamu wa Rais alipata taarifa kuhusu makampuni ya Japan ambayo yana nia ya kuwekeza Tanzania na kuelezwa namna yalivyojipanga kushirikiana na Tanzania kutimiza azma zao za uwekezaji na pia akatumia nafasi hiyo kuwaeleza kuwa Tanzania inashukuru kuona Japan ikitangaza fursa za uwekezaji nchini Tanzania. Pia aliufahamisha uongozi wa wizara hiyo kuwa kwa sasa kuna ushindani mkubwa wa kiuwekezaji nchini Tanzania hasa katika sekta za mafuta na gesi na hivyo kazi ya Tanzania ni kutazama fursa ambazo zitakidhi matakwa ya Wananchi wake na kutoa nafasi kwa makampuni ya kigeni yanayotambua na kuthamini sera za uwekezaji zilizopo nchini huku yakiwa radhi kuchangia katika kupunguza umaskini nchini badala ya kutafuta faida peke yake. “Nafahamu kampuni kutoka Japan zina nia njema ya kustusaidia kukabiliana na umaskini wa wananchi wetu, tunashukuru sana kwa moyo huo na karibuni kuwekeza Tanzania,” alisema.

Baada ya kikao hicho Mheshimiwa Makamu wa Rais alipata fursa ya kufanya mazungumzo na Mwenyekiti wa JETRO, Hiroyuki Ishige, ambaye aliongozana na baadhi ya viongozi wa kampuni hi yo na kuzungumzia nia ya Japan kutanua uwekezaji wa makampuni yao nje ya Japan, sambamba na Makampuni ya Nje kuwekeza Japan. 

Uongozi wa JETRO ulieleza nia yake ya kufungua ofisi ya kuhamasisha uwekezaji nchini Tanzania na ukafafanua kuwa mazungumzo ya kufikia lengo hilo yanaenda vizuri huku wakimtaka Mheshimiwa Makamu wa Rais kuendelea kuwasaidia ili wafanikishe azma hiyo. Balozi wa Japan nchini Tanzania, Masaki Okada, alifafanua kuwa ujio wa JETRO nchini Tanzania utafungua ukurasa mpya katika uwekezaji na pia utasaidia nchi hizi mbili kudumisha uhusiano wake ambao sasa unaakisi katika masuala ya teknolojia na uchumi.

Sambamba na hilo, Mheshimiwa Makamu wa Rais alipata nafasi ya kukutana na Ujumbe kutoka JICA, ulioongozwa na Rais wake, Akihiko Tanaka,  ambao uliishukuru serikali ya Tanzania kukubaliana  na miradi mbalimbali wanayoitekeleza nchini Tanzania huku akisisitiza umuhimu wa kukuza ushirikiano baina ya nchi hizi mbili ili wananchi wa nchi zote wazidi kunufaika. 

Kwa upande wake Mheshimiwa Makamu wa Rais ambaye katika ziara hii ameambatana na Waziri wa Uchukuzi Dk. Harrison Mwakyembe alifafanua kuwa, Tanzania inathamini uhusiano wake na Japan sambamba na mchango wake katika sekta mbalimbali na kwamba Tanzania ina tamaa kubwa ya kuona urekebishaji wa miundombinu yake hasa Reli ya Kati maeneo ambayo yamekabidhiwa kwa Japan yanafanyiwa kazi kwa wakati ili kukuza uchumi wa Tanzania na nchi jirani zinazotegemea Bandari ya Dar es Salaam katika kupitisha mizigo yake.