SIKIKA Wataka Wabunge Kupata kwa Wakati Vitabu vya Makadirio ya Bajeti

Bungeni

Bungeni

Na Mwandishi Wetu

KUTOA kwa wakati vitabu vya bajeti ya taifa kwa wabunge na umma kwa ujumla ni hatua muhimu katika kukuza uwazi, ubora na ufanisi katika bajeti. Kwa mujibu wa Ibara ya 96 ya Kanuni za Kudumu za Bunge (Toleo la mwaka 2007) Serikali inapaswa kuwapa Wabunge nakala za vitabu vya makadiirio ya bajeti angala siku 21 kabla ya kuanza kwa vikao vya bajeti kuanza.

Kwa mwaka huu, kikao cha bajeti kinatarajiwa kuanza tarehe 6 May, 2014 wakianza kukutana kamati mbalimbali tarehe 28 hadi 04 may. Hata hivyo, kwa mujibu wa mawasiliano yaliyofanyika kwa baadhi ya wabunge siku ya Ijumaa ya tarehe 25, 2014, kuna ushahidi wa wazi kwamba bado hawajapokea nyaraka muhimu kadiri ya kanuni.

Itambulike kwamba, kwa mwaka jana makadirio ya matumizi yalichapishwa katika kurasa zaidi ya 1006. Hivyo, kuchelewa kukabidhiwa kwa vitabu vya makadirio ya bajeti kwa wabunge kunaweza kuathiri kazi yao ambayo ni kuchambua mipango ya fedha, nahivyo kusababisha ugumu katika kupata maoni toka kwa wananchi wanaowawakilisha.

Zaidi ni kwamba, wanaweza kuwa katika hatari ya kupitisha makadirio ya bajeti isiyo kidhi mahitaji ya wananchi Katiba ya Tanzania, vifungu namba 63 na 137 vimelipa Bunge mamlaka, kwa niaba ya wananchi “kusimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote” kabla ya kutimiza jukumu la kisheria na kuidhinisha rasmi matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha unaofuata. Ili kutekeleza kiufanisi kazi yao ya kuidhinisha matumizi ya bajeti, wabunge wanahitaji muda wa kutosha wa kupitia nyaraka hizo na kujadili na wananchi wao, ambao kimsingi ndio wenye mamlaka juu ya serikali.

Nia miongoni mwa mambo mengine ni kuona kama vipaumbele vya wananchi vimehusishwa na kujitosheleza au kama kunahitajika kufanyika kwa marekibisho Bunge linapaswa kudai kukabidhiwa vitabu vya makadirio ya bajeti kwa wakati ili kutoa nafasi kwa ajili ya mashauriano na wananchi na kurekebisha bajeti ipasavyo, kabla ya kuidhinisha. Kadhalika, serikali lazima kuwajibika na kutoa kwa wabunge vitabu vya makadirio ya bajeti ili kuepuka kupitisha bajeti ya vitu ambavyo haikidhi mahitaji halisi.

Tunaamini kwamba kuwasilishwa kwa wakati vitabu vya makadirio ya bajeti kutawasaidia wabunge kutekeleza jukumu lao la kikatiba na kuishauri serikali jinsi ya kutumia rasilimali za taifa kwa manufaa “ya watu na kuondoa umaskini, ujinga na maradhi” (Katiba kifungu 9).

Imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Sikika, Bw. Irenei Kiria