Uchaguzi Mdogo wa Madiwani Arusha Wageuka Vurugu Tupu

Masanduku ya kupigia kura

UCHAGUZI mdogo katika kata nne za Jiji la Arusha unafanyika leo, huku Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), ikiwapiga marufuku Mkuu wa Mkoa, Magessa Mulongo na Mkuu wa Wilaya ya Arusha, John Mongella kuingia kwenye vituo vya kupigia kura, wala kujihusisha kwa namna yoyote na zoezi la upigaji kura ikisema siyo jukumu lao kisheria.

Mbali ya NEC kupiga marufuku viongozi hao wa kisiasa kukaribia vituo hivyo, uchaguzi huo umekumbwa na matukio kadhaa likiwamo la Mbunge wa Jimbo la Arusha, Godbless Lema pamoja na Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Taifa Chadema(Bavicha), John Heche, kunusurika kuswekwa rumande jana.

“RC na DC hawana haki wala mamlaka ya kujihusisha kwenye zoezi na shughuli za upigaji kura. Mwenye dhamana, wajibu na haki ya shughuli zote za upigaji kura ni Mkurugenzi wa Jiji ambaye ni mwakilishi wa NEC pamoja na maofisa wengine wanaotambuliwa kisheria,” alisema Mwenyekiti wa NEC Jaji Damian Lubuva jana.

Lema na Heche walinusurika kuswekwa rumande baada ya kufika Kituo Kikuu cha Polisi jijini Arusha, wakishinikiza jeshi hilo, kukamata magari matatu waliyodai kuwa ni ya Chama Cha Mapinduzi(CCM) na kubadilishwa namba yakihofiwa kwamba huenda yakatumika kuvuruga uchaguzi wa leo. Tukio hilo la aina yake, lilitokea jana asubuhi baada ya viongozi hao, kufika polisi na kutoa taarifa hiyo, wakieleza kuwa lakini waliambiwa waondoke kwa kuwa gari kubadili namba siyo kosa ambapo pia walitakiwa kumtaja aliyewaeleza kama magari hayo yatatumika kufanya uhalifu.

Aidha, viongozi wa vyama vyote vya siasa ambao sio mawakala wala wagombea, wamepigwa marufuku kuingia kwenye vituo vya kupigia kura, wala kujihusisha kwa namna yoyote na zoezi la upigaji kura badala yake wakiwa ni wakazi wa kata husika kupiga kura na kuondoka maeneo hayo.

Mwenyekiti wa NEC, alitoa tamko la kuzuia viongozi hao jana alipozungumza na waandishi wa habari kuelezea mipango na mikakati ya tume yake katika kufanikisha zoezi hilo linalofanyika baada ya kuahirishwa mara mbili.

Mbele ya makamu wake Jaji Mkuu mstaafu wa Zanzibar, Jaji Hamid Mohamoud Hamid, Jaji Lubuva alitaja orodha ya watu 12 wenye haki kisheria kuingia kwenye vituo vya kupigia kura na kujihusisha na zoezi la upigaji, kuhesabu, kujumlisha kura kuwa ni msimamizi wa kituo, msimamizi msaidizi wa kituo, mawakala wa vyama na wapiga kura.

Wengine ni Mkurugenzi wa Uchaguzi, mgombea, mjumbe wa NEC, Ofisa wa NEC, Mratibu wa NEC mkoa, askari polisi au mtu yeyote anayehusika na usalama katika kituo cha kupiga kura, mtu anayemsaidia mpigakura asiyejiweza na mwangalizi wa uchaguzi aliyeidhinishwa na NEC kimaandishi na katika utaratibu uliowekwa. Uchaguzi huo unafanyika leo baada ya kuahirishwa Juni 16, mwaka huu, baada ya bomu la kutupa kwa mkono kulipuka kwenye mkutano wa Chadema wa kufunga kampeni kwenye Viwanja vya Soweto, Arusha.

Agizo la kupiga marufuku kujihusisha na Uchaguzi Mkuu wa Mkoa(Mulongo) na Mkuu wa Wilaya(Mongella) ambao ni makada na wajumbe wa Kamati za Siasa na Halmashauri za Mkoa na Wilaya za CCM, limekuja wakati kukiwa na tuhuma kutoka kwa vyama vya upinzani, hasa Chadema kuwa wanatumia nyadhifa zao kukibeba chama tawala.

Akizungumzia kunusurika kuwekwa rumande, Heche alisema kutokana na majibu ya polisi wao wakiomba wapewe hata fursa ya kuandika maelezo kuhusu tukio hilo au wapewe polisi kwenda kuzikamata gari hizo, lakini waligomewa, ndipo likatolewa agizo la kukamatwa kuwekwa rumande kwa Lema.

“Mimi niligoma nikasema kwa nini akamatwe wakati tunaleta wote taarifa hapa basi watukamate wote, jukumu la polisi ni kuchunguza kwa kuwa sisi tuna taarifa magari hayo yatatumika kuteka vijana wetu na kuvuruga uchaguzi,”alisema Heche.

Alitaja magari hayo (namba tunazo) kuwa moja ni la CCM Wilaya ya Arusha na magari mengine mawili. Katibu wa Chadema Kanda ya Kaskazini, Aman Golugwa alisema kuwa wanashangazwa na polisi kukataa kukamata magari hayo na kwamba katika uchunguzi wao wamebaini moja ya namba mpya za magari hayo ni za moja ya kampuni ya nje ya Arusha.

“Tumeshangaa, badala ya polisi kuchunguza wanataka kukamata viongozi wetu, kweli hii ni halali?”alihoji Golugwa.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas hakupatikana jana kuzungumzia tukio hilo, baada ya simu yake kupigwa bila majibu huku ikielezwa kuwa alikuwa wilayani Monduli katika sherehe za kutoa kamisheni wanajeshi wa Chuo cha Maofisa wa Jeshi Monduli(TMA), ambapo Rais Jakaya Kikwete alikuwapo na viongozi wengine.

NEC ‘yahamishia’ ofisi Arusha
Tume ya Taifa ya uchaguzi (NEC), ‘imehamishia’ kwa muda ofisi zake jijini Arusha kuhakikisha zoezi la kura katika Kata za Themi, Kimandolu, Elerai na Kaloleni linafanyika kwa ufanisi.

Pamoja na Mwenyekiti wa wa NEC, Makamu wake, makamishna wanne na Mkurugenzi wa NEC, Julius Mallaba pia wapo Arusha kusimamia zoezi hilo. Makamishna wa NEC waliopo Arusha ni Jaji wastaafu John Mkwawa, Mary Longway, Profesa Amon Chariga na Mchaka Mchanga, walioambatana na watendaji kadhaa wa tume hiyo kutoka Dar es Salaam.

Akijibu swali la kwa nini wote wako jijini Arusha, Jaji Lubuva alisema wingi na uwepo wao umetokana na hali na mazingira halisi ya siasa za Jiji la Arusha kwa kuzingatia sababu za uchaguzi huo kuahirishwa mara mbili Juni 16 na 30, mwaka huu.

“Pamoja na ukweli kwamba Mkurugenzi wa Jiji ndiye msimamizi wa uchaguzi akisaidiana na watendaji wengine, mimi na makamishna wengine wa NEC tuko hapa kwa ajili ya kusimamia utendaji, kutoa ushauri na ufafanuzi kwa karibu zaidi pale jambo lolote linapojitokeza,” alisema Jaji Lubuva.

Wapiga kura kutoruhusiwa kukaa karibu na vituo vya kura
Akizungumzia maandalizi na taratibu zitakazotumika leo, Jaji Lubuva alisema wapiga kura wanashauriwa kurejea nyumbani kusubiri matokeo mara baada ya kupiga kura, badala ya kukaa karibu na vituo ili kuepuka mikusanyiko kutokana na Jiji la Arusha kukumbwa na milipuko ya mabomu.

Hata hivyo, wakati Jaji Lubuva akiwataka wananchi kuepuka mikusanyiko kwa hofu ya mabomu, mkutano mkubwa wa Injili unaohubiriwa na Askofu Emanuel Lazaro unaendelea katika Viwanja vya Sheikh Amri Abeid.

Karatasi za kura na fomu za matokea zabadilishwa rangi
Kutokana na zoezi la kupiga kura Arusha kuahirishwa Juni 16, mwaka huu baada ya karatasi za kura na fomu za matokeo kusambazwa, Jaji Lubuva alisema NEC imebadilisha rangi za karatasi hizo na fomu za matokeo kuepuka udanganyifu na hujuma yoyote.

Taarifa zinasema NEC imelazimika kubadilisha karatasi za kura na fomu za matokeo baada ya baadhi ya karatasi za kura za awali kudaiwa kupotea katika mazingira ya kutatanisha na hazipatikana hadi leo.

Kauli ya Chadema kuhusu wapigakura kurejea majumbani

Chadema kimekataa ushauri wa NEC wa kutaka wananchi kurejea nyumbani baada ya kupiga kura, badala yake kimesisitiza kuwa wafuasi wa chama hicho watakaa umbali wa zaidi ya mita 100 kutoka vituo vya kupigia kura kama sheria inavyoelekeza.

CHANZO: www.mwananchi.co.tz