Benki ya dunia kuendelea kuisaidia Zanzibar

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, akisalimiana na Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia, John M. Mclntire, aliyefika Ikulu Mjini Zanzibar leo kumuaga Rais, baada ya kumaliza muda wake wa kazi hapa nchini.


Na Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

BENKI ya Dunia imeahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi yake ya maendeleo na kueleza matumaini yake kutokana na juhudi zinazochukuliwa na serikali katika kuimarisha uchumi na huduma za kijamii.

Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia, John Mclntire aliyasema hayo leo wakati alipofika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kuaga na kuzungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein.

Katika mazungumzo yake, McIntire alimueleza Dk. Shein kuwa Benki ya Dunia inathamini juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuziimarisha sekta zake za maendeleo hatua ambayo Benki hiyo imeingia moyo kuisaidia Zanzibar.
Alisema kuwa Benki ya Dunia itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katikia kuimarisha sekta zake za maendeleo kwa kutambua malengo yaliyowekwa katika kuimarisha uchumi na maendeleo hapa nchini.

Bwana McIntire ametoa shukurani kwa serikali ya Mapinduzi Zanzibar na uongozi wake kwa kutoa mashirikiano makubwa ambayo yameweza kufanya kazi zake kwa ufanisi katika kipindi chote cha miaka minne aliyofanyakazi hapa Tanzania.
Aidha, katika maelezo yake Mkurugenzi huyo Mkaazi alimueleza Dk. Shein matumaini yake makubwa kwa Zanzibar katika kujiletea maendeleo.

Naye Dk. Shein alitoa pongezi kwa Benki ya Dunia kwa kuendelea kushirikiana vyema na Zanzibar hatua ambayo imepelekea kupata maendeleo na mafanikio makubwa katika miradi ya maendeleo. Alisema kuwa juhudi za Mkurugenzi huyo zimeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa uimarishaji wa miradi ya maendeleo hapa Zanzibar na kutoa pongezi zake za dhati kutokana na jitihada zake hizo.

Dk. Shein alisema kuwa Bwana McIntire amefanya kazi kubwa katika uongozi wake kwenye Benki hiyo hapa Tanzania na kueleza kuwa juhudi zake zitaendelea kuthaminiwa na kukumbukwa licha ya yeye kutokuwepo nchini.

Aidha, Dk. Shein alimueleza Mkurugenzi huyo kuwa viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa pamoja wamedhamiria kufanya kazi kwa mashirikiano na juhudi kwa lengo la kuiletea maendeleo Zanzibar kwa kuelewa kuwa mabadiliko ni suala la lazima.
Dk. Shein alieleza kuwa miongoni mwa mabadiliko hayo ni pamoja na kuhakikisha miradi yote ya maendeleo wanaisimamia vilivyo na kwa umahiri mkubwa kutokana na kutambua umuhimu wake katika maendeleo ya nchi na wananchi wake.

Benki ya Dunia imeweza kushirikiana na Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na mradi wa Mradi wa Uhufadhi wa Mazingira ya Bahari na Viumbe wa Baharini MACEMP, TASAF, Mradi wa BEST na miradi mengineyo.
Pia, Benki ya Dunia imekuwa mstari wa mbele katika kushirikiana na Zanzibar kwenye kuendeleza mradi wa ujenzi wa skuli mpya za kisasa za Sekondari Unguja na Pemba ambazo zimefikia hatua nzuri ya ujenzi ambapo.

Sambamba na hayo Benki ya Dunia ilitoa ushirikiano wake mkubwa katika ujenzi wa njia ya kurukia na kutulia ndege katika kiwanja cha ndege cha Abeid Amani Karume Zanzibar. Aidha, Benki ya Dunia imeweza kuunga mkono ujenzi wa miundombinu ya barabara zikiwemo barabara za ndani ya mji wa Zanzibar na zile za nje ya mji ikiwemo barabara ya Mahonda-Kinyasini na Mkwajuni-Mkokotoni.