Mbunge wa CCM amchongea DC Kwa Pinda

Mbunge wa CCM, Amos Makalla

Dodoma

MBUNGE wa Jimbo la Mvomero mkoani Morogoro , Amosi Makalla (CCM), amemuomba Waziri Mkuu Mizengo Pinda kumchukulia hatua Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Fatma Mwassa, kwa madai amegoma kugawa chakula cha msaada kilihotolewa na Serikali.

Makalla amesema kuwa ni jambo la kusikitisha kuona Serikali inatoa chakula kwa ajili ya wananchi wake halafu Mkuu wa Wilaya anazuia yasigawiwe kwa wananchi hivyo ni bora Waziri Mkuu akachukua hatua ili yaweze kugawiwa kwa walengwa.

Akizungumza wakati akichangia bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu juzi, mjini hapa ,Makalla alisema Serikali imetoa tani 86 za chakula kwa ajili ya wananchi wa wilaya hiyo lakini hadi sasa bado hawajapewa walenga.

Makalla katika shutuma hizo dhidi ya Mwasa alisema kuwa April mwaka huu, Serikali iliamua kutoa tani hizo 86 za chakula kwa wananchi wa Wilaya ya Mvomero waliokuwa katika Kata za Kanga, Diongoya, Mzumbe, Mvomero, Doma, Mlali na Melela.

Alisema kwa mujibu wa Serikali , tani 8.6 kati ya hizo, zigawiwe bure kwa wananchi wenye njaa na tani 77.4 ziuzwe kwa wananchi kwa bei ya Sh 50 kwa kilo moja.

Aliongeza kuwa kutokana na utaratibu huo,Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya wilaya April 29 mwaka huu, lilikaa na Mkurugenzi wa wilaya akatumia nafasi hiyo kuomba tani 8.6 zigawiwe katika kata saba na tani 77.4 ziuzwe katika kata hizo hizo.

Mbunge huyo ambaye amekua na ari kubwa ya kuwasemea wananchi wake tangu alipochaguliwa katika Uchaguzi Mkuu mwaka jana alimbwambia Pinda kuwa baada ya kusikia taarifa hizo aliliomba baraza la madiwani limkubalie kulipia tani 77.4 za chakula hicho ili wananchi wake mpa tani “Niliposikia hivyo, mimi nikaliomba baraza la madiwani linikubalie kulipia tani 77.4 za chakula hicho ili akagawe kwa wananchi.

“Baraza likakubali, Mei 9 mwaka huu, nikaweka katika akaunti ya Halmashauri ya Wilaya sh.milioni 3, 780,000 kwa ajili ya kulipia chakula ili wananchi wangu wasipate taabu.Cha kusangaza DC alipopata taaria akaamua kuzuia chakula hicho kisigawiwe bure kwa madai nitapa umaarufu.

“Kutokana na hali hiyo akaamua kutoa maagizo kuwa chakula hicho kiuzwe kama livyokuwa imepangwa awali na akasema nirudishiwe fedha ambazo nilikuwa nimetoa kwa ajili ya kununua chakula hicho kwa lengo la kuwasaidia wananchi wangu,”alisema Makalla.

Alisisitiza Juni 1 mwaka huu, mkurugenzi akawaandikia barua watendaji wa kata kuwaeleza namna ya kuuza chakula hicho.Hata hivyo watendaji hao waliamua kukataa kwa sababu alipokubaliwa kupewa chakula hicho nao walikuwepo na wanashangaa kwanini wanapewa maelekezo tofauti nay a awali.

“Ni uamuzi wa ajabu sana ambao DC aliamua kuuchukua, lakini nachokuomba Waziri Mkuu mchukulie hatua kwa sababu alichokifanya si kizuri na wala hakileti picha nzuri kwa Serikali yetu sikivu,”alisema Makalla.

Alifafanua kuwa Serikali inapoama kutoa msaada wa chakula kwa ajili ya wananchi wake lengo linakuwa zuri lakini kitendo cha baadhi ya watendaji katika wilaya kukwamisha msaada huo ni jambo ambalo halipaswi kuvumilika na ndio maana akatumia nafasi hiyo kumuomba Waziri Mkuu Pinda kumuwajibisha.

CHANZO; Jambo Leo