Mali: Mwanajeshi auwawa Timbuktu

MWANAJESHI mmoja wa Mali ameuwawa katika shambulizi la kigaidi katika mji wa kihistoria wa Timbuktu.

Taarifa kutoka jeshi la Mali imesema kuwa shambulizi hilo lilitekelezwa na gaidi aliyekuwa ndani ya gari na amevalia kilipuzi.

Dereva wa gari hilo alipofika katika kizuizi cha barabarani karibu na uwanja wa ndege alijilipua na kusababisha kifo cha mwanajeshi huyo mmoja.

Hii ni mara ya kwanza kwa shambulizi la kujitolea muhanga kutokea katika mji huu wa Timbuktu tangu jeshi linaloongozwa na Ufaransa kuwatimua wanamgambo wa kiislamu kutoka mji huo mwezi wa Januari.

Lakini jeshi la Ufaransa limetangaza kwamba liliwauwa wanamgambo 10 katika makabiliano yaliofanyika baada ya shambulizi hilo la kigaidi.

Wakati huo huo Serikali ya Ufaransa imesema kwamba bado inajaribu kuthibitisha taarifa kutoka kwa magaidi wa Al qaeda walioko eneo la Maghreb(AQIM) kwamba walimuuwa mateka wa kifaransa Bwana Philippe Verdon tarehe 10 Machi ili kulipiza kisasi hatua ya Ufaransa kuingia Mali.

Majeshi ya Ufaransa yaliingia nchini Mali katika harakati za kijeshi za kuyakomboa maeneo ya kaskazini yaliokuwa wakati huo chini ya udhibiti wa wanamgambo wa kiisalmu.

Ufaransa imejitetea mara kadhaa ikisema ililazimika kuingia nchini Mali kuzuia magaidi kubuni taifa la kigaidi.

-BBC