Wachezaji 1,200 watoto kushiriki tamasha

Ofisa Habari wa TFF, Boniface Wambura

Na Mwandishi Wetu

WACHEZAJI mpira wa miguu (wasichana na wavulana) wenye umri kuanzia miaka 6-12 kutoka Mkoa wa Dar es Salaam watashiriki katika tamasha (festival) litakalofanyika Desemba 17 mwaka huu Uwanja wa Taifa.

Akitoa taarifa hiyo kwa vyombo vya habari leo Dar es Salaam, Ofisa Habari wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Boniface Wambura amesema tamasha hilo litatanguliwa semina itakayoshirikisha walimu 30 (15 wa kiume na 15 wa kike) na kufanyika ofisi za TFF kuanzia Desemba 14-16 mwaka huu.

Alisema, semina hiyo itakuwa chini ya Mkufunzi kutoka Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) na kila shule (maalumu zilizoteuliwa) zitatoa kila moja wanafunzi kati ya 30-40.

Wakati huo huo, Wambura amesema kozi ya ukocha kwa ajili ya Leseni B ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) inatarajia kufanyika Dar es Salaam Desemba 19-22 mwaka huu, ambapo itashirikisha makocha 40 wenye cheti ya ngazi ya juu (advance) kutoka sehemu mbalimbali nchini.

Aidha amefafanua kuwa mkufunzi kutoka CAF ndiye atakayeendesha kozi hiyo ambayo itakuwa ya pili kufanyika nchini baada ya ile ya Leseni C iliyofanyika kuanzia Novemba 7-20 mwaka huu. Kozi ya Leseni C ilishirikisha makocha 28 kutoka sehemu mbalimbali nchini ambapo wote walifaulu

Pamoja na hayo ameongeza kuwa Semina nyingine na mtihani wa utimamu wa mwili (physical fitness test) kwa waamuzi (Group C) itafanyika katika vituo vitatu tofauti kuanzia Desemba 18-20 mwaka huu.

Vituo ambavyo semina hiyo itafanyika ni Dodoma, Mwanza na Songea. Desemba 18 na 19 mwaka huu itakuwa ni semina wakati physical fitness test itafanyika Desemba 20 mwaka huu.

Akizungumzia Semina kwa Makamishna wa ngazi ya juu (elite) wanaosimamia Ligi Kuu, Ligi Daraja la Kwanza na mashindano mengine yanayosimamiwa moja kwa moja na TFF amedai itafanyika Desemba 28 na 29 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Semina hiyo ni maalumu kwa wale ambao walikosa semina iliyopita. Pia washiriki ambao hawakufanya vizuri kwenye semina iliyopita wanatakiwa kuhudhuria.