Dk. Bilal aiwakilisha Tanzania Mkutano wa Wakuu wa nchi EAC

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohammed Gharib Bilal, akisalimiana na Balozi wa Tanzania, nchini Burundi, Dkt. James Mwasi, baada ya kuwasili kwenye ukumbi wa Golf kwa ajili ya kufunga Mkutano wa Nchi za Maziwa Makuu, uliokuwa ukijadili Uendelezwaji wa Ukanda wa Ziwa Tanganyika, uliomalizika Novemba 29, Bujumbura Burundi. (Picha na Muhidin Sufiani-OMR)

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mohammed Gharib Bilal ameiwakilisha Tanzania katika Mkutano wa Wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) unaofanyika mjini Bujumbura, Burundi kuanzia Novemba 29 na 30, 2011.

Makamu wa Rais amewasili mjini hapa jana ambapo alipokelewa na mawaziri kadhaa wa Tanzania waliotangulia kuhudhuria mikutano ya ngazi za mawaziri, wakiongozwa na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, Waziri wa Ulinzi Dk. Hussein Mwinyi, manaibu Waziri, Deo Mfutakamba, Lazaro Nyalandu na Adam Malima.

Kwa mujibu wa taarifa mikutano ya awali ngazi ya mawaziri, kwa kushirikiana na nchi nyingine za ukanda huu, wamejadili namna ya kusaini Protokali ya Ulinzi wa pamoja, protokali inayotaka nchi wanachama wa Jumuiya hii kushirikiana kijeshi pale inapokubalika ama inapoonekana kufaa baada ya nchi mwanachama kuwa katika hatari ya vita.

Waziri wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, akiwa katika Ukumbi wa Golf, wakati akimsikiliza kwa makini Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Mohammed Gharib Bilal, alipokuwa akifunga rasmi Mkutano wa Nchi za Maziwa Makuu, uliokuwa ukijadili Uendelezwaji wa Ukanda wa Ziwa Tanganyika, uliomalizika Novemba 29, Bujumbura Burundi. Picha na Muhidin Sufiani-OMR


Hata hivyo mjadala huu ulikuwa ni mkali huku Tanzania ikitaka protokali hii isainiwe mara tu pale itakapokuwa na kipengele kinachobainisha kuwa, nchi wanachama watatakiwa kushirikiana ama kusaidiana baada ya kila nchi mwanachama kupima aina ya hatari na mchango wa hatari hiyo kwa nchi mshiriki ambaye ni mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Pia, mkutano huu ulikuwa na kazi ya kupitisha maelekezo ya wataalam yanayolenga kuongeza kasi ya kuundwa kwa shirikisho la Afrika Mashariki. Msimamo wa Tanzania katika agenda hii ni kuwa zoezi hili halijafikia muda muafaka na kwamba kuna mambo mengi yanayotakiwa kufanyika kabla ya Jumuiya hii kuunda shirikisho.

Hata hivyo nchi nyingine za Afrika Mashariki zimekuwa zikishirikiana kwa lengo la kuongeza kasi na kuishinikiza Tanzania kukubali kuundwa kwa shirikisho, jambo ambalo linapingana na taratibu na kanuni za Jumuiya hii, zinazotokana maamuzi yote yafanyike kwa makubaliano yanayotoka kwa wananchi wa jumuiya hii na kwa kila taifa husika. Kwa mujibu wa ujumbe wa Tanzania, suala la shirikisho lilipingwa katika kamati ya Wangwe na hadi wakati Tume hiyo ilipokusanya maoni, hadi sasa hakujawa na tofauti ya mtazamo.

Tanzania inahitaji kufanyika kwanza maafikiano katika soko la pamoja na mataifa ya jumuiya hii kutazama namna yatakavyoweza kunufaika kabla ya kukimbilia ushirikiano wa kisiasa ambao kama utakimbiliwa bila mazingira kujengwa, ni rahisi kwa jumuiya hii kuvunjika kama ilivyowahi kufanyika huko nyuma.

Makamu wa Rais pia alikuwa na kazi ya kufunga mkutano wa nchi za Maziwa Makuu uliokuwa ukijadili mahusiano na uendelezaji wa Ukanda za Ziwa Tanganyika ambapo katika mkutano huo, alifafanua namna Tanzania inavyoshiriki kwa ukamilifu kuunganisha mikoa yake na nchi za mipakani hasa katika ujenzi wa barabara za lami, na namna ushirikiano kati ya nchi za SADC, EAC na COMESA unavyolenga kukuza biashara sambmba na uchumi kwa nchi wanachama.

Makamu wa Rais anarejea nyumbani kesho Desemba Mosi ambapo atakuwa na kazi ya ufunguzi wa barabara jijini Dar es Salaam Desemba pili, 2011.