Wahadhiri watano UDSM wawa maprofesa

 

Balozi Fulgence Kazaura, akitunuku cheti kwenye moja ya mahafali ya Chuo Kikuu Cha DSM.

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), kimeongeza idadi ya maprofesa, baada ya Baraza lake kuidhinisha kupandishwa vyeo kwa wahadhiri wake watano kuwa maprofesa kamili na maprofesa washiriki.

Hatua hiyoilifikiwa katika kikao baraza hilo cha 204, kilichofanyika juzi jijini Dar es Salaam.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyosainiwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo hicho Taaluma, Profesa Makenya Maboko, ilimtaja aliyepandishwa kuwa Profesa kamili kuwa ni aliyekuwa Profesa Mshiriki, Geofrey John, kutoka kwenye Chuo cha Uhandisi na Teknolojia.

Waliopandishwa kuwa maprofesa washiriki, ni wahadhiri waandamizi, Dk. Herbert Lyaluu, Dk. Richard Kangalawe, Dk. Alex Mrema na Dk. Audax Mabula.

Taarifa hiyo ilisema wasomi hao walipandishwa vyeo hivyo, kuanzia Julai Mosi, mwaka huu.

Hii ni mara ya pili ndani ya mwaka huu chuo hicho kinapata maprofesa kamili na maprofesa washiriki.

Julai 28, mwaka huu, Baraza la Chuo hicho liliidhinisha pia kupandishwa vyeo kwa maprofesa washiriki wawili kuwa maprofesa kamili na wahadhiri waandamizi tisa kuwa maprofesa washiriki.

Walioidhinishwa katika kikao hicho kuwa maprofesa kamili ni Profesa Mshiriki, John Machiwa kutoka Chuo cha Sayansi ya Asili na Samwel Manyele wa Chuo cha Uhandisi na Teknolojia.

Wahadhiri Waandamizi walioidhinishwa kuwa maprofesa washiriki katika kikao hicho, ni Dk. Bernadeta Killian, Dk. Sylivia Temu, Dk. Agnes Mwakaje, Dk. Hussein Sosovele, Dk. Estomih Massawe na Dk. Emrod Elisante.

Wahadhri waandamizi wengine, ni Dk. Amos Majule, Dk. Michael Wambali na Dk. Joseph Buchweishaija.

CHANZO: NIPASHE